Na; Milka Kaswamila-Afisa Habari-Mlimba DC
Kitengo cha Maliasili na Uhifadhi wa Mazingira cha Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, kimekemea vikali uchimbaji holela wa vifusi, uharibifu wa mto Mngeta pamoja na kuahidi kudhibiti nyani waharibifu katika Shule ya Sekondari Kiburubutu, iliyopo Kata ya Mngeta.
Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkuu wa Kitengo hicho, Ndg. Jaji Mafuru Machumu, alipokuwa akiongoza timu ya wataalamu kutoka sekta za mazingira, misitu na nyuki katika ziara ya ukaguzi wa utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku, iliyohusisha mto Mngeta, Shule ya Sekondari Kiburubutu na eneo ambalo wananchi wameanza kuchimba vifusi kiholela katika Kijiji cha Kidete, karibu na Shule ya Sekondari Mchombe.
Akiwa Kijiji cha Kidete, Ndg. Mafuru amesema wataalamu hao wamebaini uwepo wa shimo la kifusi lililochimbwa kiholela na wananchi binafsi ndani ya umbali wa mita 60 kutoka reli ya TAZARA, hali inayoweza kusababisha mmomonyoko wa udongo, kuhatarisha usalama wa reli hiyo pamoja na kuharibu mazingira kwa ujumla.
Kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, amewataka wananchi kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za uchimbaji wa vifusi, ikiwemo kupata vibali halali kutoka Ofisi ya Kijiji husika, ambako Mtendaji wa Kijiji ndiye mwenye mamlaka ya kutoa vibali hivyo.
Katika Shule ya Sekondari Kiburubutu, wataalamu hao walioneshwa maeneo ambayo nyani huvamia na kusababisha usumbufu shuleni, ambapo wameahidi kuandaa mikakati ya muda mfupi na mrefu ya kudhibiti tatizo hilo.
Wakati wa ziara yao katika mto Mngeta, ambao ni mojawapo ya vyanzo muhimu vya maji kwa mto Kilombero, wataalamu hao walibaini kuwa shughuli za kilimo na usafirishaji zinafanyika ndani ya mita 60 kutoka kingo za mto, hali inayochangia uharibifu wa mazingira ya mto huo. Kutokana na hali hiyo, wameazimia kuendelea kutoa elimu ya uhifadhi wa misitu kwa wananchi wa vijiji vya Mngeta na Itongowa ili kuhakikisha misitu inaendelea kulindwa na vyanzo vya maji vinahifadhiwa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Awali, kabla ya kufika mto Mngeta, timu hiyo ilitembelea Ofisi za SUMA JKT (KPL) kwa ajili ya kujitambulisha na kujadili namna bora ya kushirikiana katika uhifadhi wa misitu inayozunguka mto Mngeta na kuudhibiti uharibifu wa mazingira ya mto huo, ikiwemo kudhibiti shughuli za kilimo kandokando ya mto huo, kutokana na umuhimu wake kwa shughuli za shirika hilo zikiwemo uzalishaji wa umeme.
MWISHO
Mngeta Kijiji cha Itongoa
Anuani: P.O.BOX 263
Simu: 023 293 1523
Mobile: 0232931523
Barua pepe: ded@kilomberodc.go.tz
Hatimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.Haki zote zimehifadhiwa